Matumaini Bado Yapo Kufanya Kazi Na DW

 

Hongera Idhaa ya Kiswahili ya DW kwa kutimiza miaka 60 ya kuhudumia wakazi na wasikilizaji wa Afrika Mashariki na Kati.

Wakati mtangazaji wa DW Josephat Charo akihitimisha kipindi maalumu cha MAONI katika kuadhimisha miaka 60 mnamo Februari Mosi, 2023 alisema, Mohammed Abdulrahman tukamilishe kipindi chetu, Februari Mosi mwaka 1963 matangazo ya Kiswahili yalizinduliwa rasmi yakilenga eneo la Afrika Mashariki na Kati, yalizinduliwa mwaka uliokuwa na makubwa ya kihistoria; Hotuba ya Rais wa Marekani wakati huo John F. Kennedy katika jiji la Berlin ambalo lilikuwa limegawanyika wakati wa enzi ya vita baridi; Kenya ni mwaka huo huo ilipata uhuru wake mikononi mwa Mwingereza na Rais wa kwanza JomoKenyatta akaja na kauli mbiu yake, wito wake wa harambee na hapa nchini Ujerumani akachaguliwa Ludwig Erhard kuwa kansela wa pili tangu kumalizika kwa Vita vya Pili vya Dunia. Maandamano ya Luther King kwenda Washington kule Marekani na hotuba yake ‘I have a Dream’ au Nina Ndoto au Nina Matumaini. Ni matumaini yapi unayaona,mustakabali wa Idhaa ya Kiswahili DW…Mohammed.”

Binafsi nikaguswa na mstari huu wakati akimtupia swali mkongwe katika utangazaji mstaafu Mohammed Abdulrahman,

Maandamano ya Luther King kwenda Washington kule Marekani na hotuba yake ‘I have a Dream’ au Nina Ndoto au Nina Matumaini. Ni matumaini yapi unayaona…..”

Kutoka katika vilindi vya moyo wangu bado matumaini yapo hai ya kufanya kazi na DW haijalishi ni lini, kwani mpaka naandika ujumbe huu kwenu DW nina umri wa miaka 38.

Tangu nikiwa mdogo, mara kadhaa nilikuwa pembeni ya Redio ya Baba yangu katika masafa ya Short Wave (SW) kusikiliza taarifa za ulimwengu kutoka Cologne.

Miaka ile ya 1990 ndoto ya kufanya kazi na Sauti ya Ujerumani ilizidi kutiwa nguvu na watangazaji waliokuwepo wakati huo.

Kudhihirisha hilo nilipokuwa darasa la sita nakumbuka nilinunua redio ndogo kwa mmachinga mmoja aliyekuwa akitembeza redio za kuuza kwa shilingi 3,000/=.

Ulikuwa mwaka mzuri sana kwangu, mwaka 1997 katika kijiji cha Lyamkena , Makambako mkoani Njombe.

Sikumwambia mama wala baba, nilimshirikisha muuza duka mmoja aliyefahamika kwa jina la Method Kiwale anipe betri mbili za BELL akaniambia anazo NATIONAL kwa ahadi ya kumlipa siku za usoni, akanipa.

Jioni ya siku hiyo mwezi wa saba sikumbuki tarehe; ilipofika saa 12:00 jioni nilikuwa shambani juu ya kichuguu kusikiliza matangazo ya Sauti ya Ujerumani-Cologne; yalipoisha nilizima kiredio changu na kukificha kwa umakini mkubwa chumbani.

Nilijiambia nafsini mwangu nitakuja kufanya kazi na Sauti ya Ujerumani. HAIJATIMIA BADO LAKINI MATUMAINI YAPO HAI.

Katika kipindi cha maoni sikumfaidi sana Othman Miraji huenda muda mwingi nilikuwa shule lakini vizuri nimemfaidi Mohammed Abdulrahman  katika mada tofauti tofauti. Kwa sasa namfaidi Mohammed Khelef na wengine. Kwa ujumla wengi wananikosha na kujihisi wamenizunguka na kuniaminisha kuwa inawezekana siku ndoto itakuwa kamili.

Nikiwa kidato cha sita huko Tabora Boys miaka ile ya 2003-2005 niliwahi kutuma barua kwa njia ya Posta kutokana na swali lililoulizwa nakumbuka lilihusu klabu ya soka Manchester United, sikujua kama barua ilifika au la … lakini nilifurahi nilipotuma DW kwa anwani waliyoitaja nami kubandika stempu kisha kuitumbukiza katika sanduku la Posta mjini Tabora.

Utaratibu wa kununua viredio vidogo uliendelea hata nilipokuwa Tabora kutokana na hamasa ninapoisikiliza DW.

Kwa mara ya kwanza kuonana na mtangazaji wa DW wakati huo akiwa ni ripota  ni HAWA BIHOGA nilifurahi sana,hiyo ilikuwa mwaka 2017.

Nilikutana naye katika Mkutano wa Wanahabari wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pale Kinondoni-Dar es Salaam wakati huo nikifanya kazi KISS FM.

Nikamuuliza ninaweza kuzungumza na Iddi Sessanga? Akaniuliza kwanini, nikamweleza…” Sauti yake inanishangaza sana”. Akampigia simu tukiwa tunaelekeza studio za Kiss FM maeneo ya Morocco-Kinondoni.

Nikazungumza na Iddi Sessanga moja kwa moja nikafurahi sana na kuyaona matumaini yangu yanazidi kukaribia huko…ila sijui lini nitafika DW…

I have a Dream to work with DW”

Ndimi

Jabir Johnson

+255 693 710 200

johnsonjabir@gmail.com


 

Post a Comment

0 Comments

Total Pageviews